![]() |
MWENYEKITI wa Bodi ya Chuo Kikuu cha
Tumaini Makumira tawi la Mbeya, Dk Owdenburg Mdegela amewapigia magoti
washarika wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) nchini kote
akiwaomba wasaidie kulipa zaidi ya Sh Bilioni 1.8 wanazodaiwa na Benki ya Biashara
ya Afrika (CBA).
Akizungumza na wanahabari juzi mjini
Iringa, Dk Mdegela ambaye ni Askofu Mstaafu wa KKKT Dayosisi ya Iringa alisema
chuo hicho ambacho ni sehemu ya kanisa hilo kipo katika hatari ya kuzama kwa
kushitakiwa na kuuziwa mali zake, hatua itakayoitia aibu KKKT.
Alisema ameamua kujilipua na kuomba
msaada huo kupitia vyombo vya habari baada ya kuona jitihada na mikutano mingi
ya kulipa deni hilo na malimbikizo yake ya riba kwa njia za kawaida za kanisa
yakipata vikwazo.
Alisema Desemba, 2013 chuo hicho kilikopa
kutoka katika benki hiyo zaidi ya Sh Bilioni 1.6 kwa ajili ya ujenzi wa jengo
la utawala na madarasa ya chuo; mkopo ambao sehemu yake haukutumika kwa kazi
iliyokusudiwa.
Bila kutaja majina ya wahusika wa
matumizi mabaya ya fedha za mkopo huo, Dk Mdegela alisema baadhi ya wajumbe wa
bodi na viongozi wa chuo hicho wanapaswa kubeba lawama na kuchukuliwa hatua za
kisheria kutokana na ubadhirifu uliofanywa.
“Tumefanya ukaguzi wa hesabu za mkopo huo
mara mbili. KKKT ilifanya ukaguzi wake lakini pia kulikuwa na mkaguzi wa nje.
Kwa pamoja wamebaini kuwepo kwa ubadhirifu mkubwa, rushwa na ufisadi” alisema.
Alisema ukaguzi wa awali unaonesha
asilimia 45 ya mkopo huo ndiyo iliyotumika kwa kazi iliyokusudiwa huku asilimia
55 iliyobaki ikitumika kwa malengo tofauti na ujenzi uliokusudiwa.
“Suala hili limeshakabidhiwa Polisi na
kwa wanasheria ili hatua za kisheria kwa wahusika zichukuliwe. Na kwa taarifa
ni kwamba wahusika wanaotuhumiwa kwa ubadhirifu huo wamekwisha simamishwa
kazi,” alisema bila kuwataja watuhumiwa hao.
Dk Mdegela ambaye pia ni mwenyekiti wa
timu ya maaskofu watatu wa kunusuru chuo hicho (Dk Mdegela, Dk Alex Malasula na
Dk Abednego Mshahara) alisema kwa makubaliano ya kulimaza suala hilo
kiungwana, benki hiyo imewataka kulipa Sh Milioni 275 ifikapo mwishoni mwa
mwezi huu na kwamba marejesho ya deni hilo yataendelea kufanywa kila mwezi.
“Mahali lilipofika suala hili sio mahali
pa kunyamaza, tunataka kila mlutheri na sharika zake zote nchini zijue
kinachoendelea na wachangie kunusuru chuo hicho ili kuliondolea kanisa aibu,”
alisema.
Alisema ili kufikia makusanyo hayo
kutakuwa na makundi manne, la kwanza litajumuisha watu watakaombwa kuchangia Sh
100,000 na kuendelea, la pili watachangia kati ya Sh 50,000 na Sh 100,000, la
tatu kati ya Sh 20,000 na Sh 50,000 na la nne kiasi chochote chini ya Sh
20,000.
Pamoja na mapendekezo hayo alisema, watu
wataruhusiwa kuchanga zaidi ya kiwango kinachopendekezwa katika makundi yao kwa
kadri watakavyoguswa na jambo hilo alilosema ni tatizo kwa kanisa.
“Lakini pia nitalazimika kukutana na
walutheri maarufu ambao ni waajiriwa katika taasisi mbalimbali, wafanyabishara
na wanasiasa na wadau wengine wa KKKT nchini,” alisema na kuwataja baadhi yao
kuwa ni pamoja na Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi na Mkurugenzi
Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk Charles Kimei.
Pamoja na kupitisha kapu hilo, alisema
wanaendelea kuandaa njia nyingine zitakazosaidia kufikia lengo la makusanyo na
marejesho ya deni hilo hadi litakapokwisha.
Dk Mdegella aliwataka wadau hao kuchangia
chuo hicho kupitia akaunti maalumu No 108433100028 iliyofunguliwa katika benki
hiyo ya CBA kwa ajili ya kukusanya na kulipa deni hilo.
Alisema yote hayo anayafanya kwa niaba ya
Mkuu wa Kanisa, Askofu Dk Frederick Shoo na kwa niaba ya askofu wa dayosisi ya
Iringa, bodi ya wadhamini ya chuo, baraza la uongozi na maaskofu wenzake na
wajumbe waliopewa kazi ya kunusuru chuo hicho.
“Kwa yoyote anayehitaji ufafanuzi zaidi anaweza kuwasiliana
wa jinsi ya kukisaidia chuo hicho anaweza kuwasiliana name kupitia simu yangu
ya mkononi namba 0754313173,” alisema.
0 comments:
Post a Comment